Home » » Mauaji ya kutisha:Acharangwa kwa sime hadi kufa na mumewe.

Mauaji ya kutisha:Acharangwa kwa sime hadi kufa na mumewe.

JESHI la Polisi Mkoa wa Arusha linamsaka kwa udi na uvumba, muuza nyama jijini hapa, Lucas Lomayany Molel (37) mkazi wa Ilboru kwa madai ya kumuua mkewe wa ndoa, Agnes Lucas (24) kwa kumcharanga na sime kwa kile kinachoelezwa kuwa ni kutokana na wivu wa mapenzi.
Dada wa Lucas Lomayany Molel (37) anayesakwa kwa kumuua mkewe wa ndoa, Agnes Lucas (24), akiwa katika chumba kilichotumika kwa mauaji hayo.
Chanzo cha habari kimeliambia Amani kuwa, tukio hilo la kutisha lilitokea usiku wa kuamkia Julai 7, mwaka huu, nyumbani kwa mtuhumiwa ambapo baada ya kutekeleza mauaji hayo aliufunika mwili wa marehemu kwa shuka na kuendelea kulala nao kitandani hadi alfajiri alipotoroka.

Akisimulia kuhusu mauaji hayo, ndugu wa marehemu aitwaye William Lomayany alisema usiku wa tukio, saa 4, mtuhumiwa alirejea nyumbani kwake na kutomkuta mkewe, akamsubiri hadi saa 6 usiku, mke akarejea.
Godoro la kitanda alipokuwa analala marehemu, Agnes likiwa limechafuka kwa damu.
Alisema marehemu baada ya kufunguliwa mlango na kuingia, alivua nguo zote na kubaki na ‘kufuli’ ambapo alijifunga kanga na kupanda kitandani kulala. Mtuhumiwa alimfuata chumbani na kumhoji kuhusu kuchelewa nyumbani hadi muda huo na ndipo mzozo ulipoanza.
William alizidi kusema kuwa, wawili hao walianza kugombana kwa maneno lakini baada ya muda hali ya utulivu ilirejea, ndipo asubuhi ilipopatikana taarifa za kuuawa kwa Agnes jambo lililotafsiriwa kuwa huenda utulivu huo tayari Agnes alishauawa.
Ndoo ikiwa na damu ya Marehemu Agnes Lucas.
Inadaiwa kuwa, mtoto wa kwanza wa mtuhumiwa, Jessica Lucas (11) ndiye aliyekuwa wa kwanza kufungua mlango wa  chumbani kwa wazazi wake na kumkuta mama yake amelala na damu chapachapa, akaenda kutoa taarifa kwa majirani.
Ilidaiwa kuwa, baada ya taarifa hiyo, majirani waliingia ndani ya chumba hicho na kuukuta mwili wa marehemu ukiwa umelala kwenye dimbwi la damu huku akiwa mtupu.
Agnes Lucas, enzi za uhai wake, akiwa kwenye picha ya pamoja na mumewe, Bw. Lucas Lomayany Molel.
Akizungumza mbele ya askari polisi waliofika kushuhudia tukio hilo, Jessica alisema baba yake alimwamsha usiku akimtaka atoke kufunga mlango baada ya kutoka ndani. Akajua baba yake anakwenda kazini kama ada.
“Nilikwenda kufunga mlango, baba aliondoka bila kusema chochote. Lakini jana usiku (Julai 6) baba alimpiga sana mama na alinipiga na mimi wakati namwambia amsamehe,” alisema Jessica.
Majirani wa wanandoa hao, wamelaani mauaji hayo na kusema Lucas hakupaswa kumuua mkewe badala yake angewashirikisha watu wengine wakiwemo wazazi wamkanye kama alikuwa akimsaliti.
“Kwa jinsi Lucas alivyokuwa mpole sikutegemea kama angemuua mkewe kikatili, kama  alikuwa akimsaliti angewaeleza wazazi wake ili wamkanye,” alisema jirani yao ambaye hakupenda jina lake liandikwe gazetini.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas alikiri kutokea kwa tukio hilo na kusema kuwa, uchunguzi  unaendelea na jeshi lake linamsaka mtuhumiwa huyo.
Share this article :
 
Copyright © March 2012. MARIDADI AGENCY
-Haki zote zimehifadhiwa
- All Rights Reserved
Template Modified by Hassan Moh Toziri
Published by Maridadi Agency