Home » » Part 3 juu ya kifo cha Billali: Hata nilivyojaribu kuwahi sikufanikiwa kumkuta kaka akiwa hai.

Part 3 juu ya kifo cha Billali: Hata nilivyojaribu kuwahi sikufanikiwa kumkuta kaka akiwa hai.



Margaret Ballali ambaye ni dada mdogo wa aliyewahi kuwa Gavana wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT), Daudi Ballali ameeleza jinsi alivyojitahidi kumuwahi kaka yake kabla ya kukutwa na mauti, lakini alishindwa na badala yake akaambulia kutoa heshima za mwisho na kushiriki mazishi.

Margaret alisema alikwenda Marekani kutokana na wito alioupokea Mei 12, 2008, saa 11:00 jioni kutoka kwa wifi yake (mke wa Ballali, Anna Muganda), akimtaka afanye haraka kwenda nchini humo kwani hali ya kaka yake (Ballali) haikuwa nzuri na kwamba alikuwa akihitaji kuzungumza naye.

“Taarifa hiyo ilinishtua sana maana wifi aliniambia nifanye nifanyavyo kutafuta ndege mapema kadri inavyowezekana ili niende, maana hali ya kaka ilikuwa mbaya, kwa hiyo nilijipanga na kwa sababu Mzee (Askofu Dk Gerald Mpango) alikuwa huko kwa shughuli za kikazi, nilimwarifu ili ikiwezekana tukutane (Washington) DC,” alisema Margaret ambaye ni mke wa Askofu Mpango wa Kanisa la Anglikana.

Alisema kutokana na kwamba alikuwa Kigoma wakati huo, ilimchukua siku tatu kuanza safari, hivyo alisafiri kwa ndege ya Swiss Air, Mei 15, 2008 na kutua Uwanja wa JF Kennedy, New York Marekani Mei 16, saa 4:00 asubuhi, siku ambayo Ballali alifariki dunia.

“Nikiwa njiani na hata baada ya kutuas JFK, nilikuwa nawasiliana na wifi. Alionekana kama mtu aliyekata tamaa na alikuwa akiniuliza niko wapi kila wakati, nilikuwa nikisubiri ndege hapo kwa saa kama mbili. Bahati mbaya ni kwamba baada ya kucheck inn (kuidhinishwa kusafiri na kuingia sehemu ya kusubiria ndege), gurudumu lake moja lilipasuka,” alisema.

“Hili jambo halikuwa la kawaida kwasababu ilibidi sasa tushuke na tusubiri tena kwa saa kama mbili ili tubadilishiwe ndege, na wakati nikiwa bado uwanjani hapo JFK, ilikuwa kama saa 8:00 mchana, nilipata simu kutoka kwa wifi akiniambia ‘Mage we have lost Daudi’ (Margaret, tumempoteza Daudi (Ballali).”

Alisema hakuwa na cha kufanya zaidi ya kuendelea na taratibu za safari na kwamba alipowasili Washington muda wa jioni alikwenda moja kwa moja kwenye nyumba ya kuhifadhia maiti ya Vo Funeral Home ambako aliwakuta wanafamilia, akiwamo Mama Muganda, watoto wa Marehemu Rahel na Octavio pamoja na wauguzi wawili na madaktari wakiwa wamezunguka kitanda cha marehemu, kabla ya mwili wake kuhifadhiwa.

Alisema baada ya hapo walirejea nyumbani na kuanza kupanga taratibu za mazishi, ambayo yalifanyika Mei 23, 2008 katika makaburi ya Gate of Heaven eneo la Silver Spring, Maryland, Marekani, huku mumewe, Dk Mpango akiwa miongoni mwa walioongoza ibada ya maziko ya kiongozi huyo.


Baadhi ya ndugu wa Ballali wanasema kubadilika ghafla na kuwa mahututi kuliwashtua kutokana na kutokuwapo kwa taarifa za mapema kuhusu ugonjwa wake.

Wanasema Ballali aliondoka Agosti 2007 kwenda Marekani akiwa mzima na hawakuwa na taarifa zozote kwamba ni mgonjwa, lakini walishtushwa na taarifa za kuugua kwake ghafla kiasi cha kuambiwa kwamba alikuwa mahututi.

Ballali alilazwa katika Hospitali ya Massachusetts, Boston mwishoni mwa Agosti 2007, wakati alipokwenda kwa ajili ya uchunguzi wa afya yake na tangu wakati huo afya yake haikuimarika hadi alipofariki dunia, Mei 16, 2008 akiwa nyumbani kwake Washington DC.
Share this article :
 
Copyright © March 2012. MARIDADI AGENCY
-Haki zote zimehifadhiwa
- All Rights Reserved
Template Modified by Hassan Moh Toziri
Published by Maridadi Agency