Home » » Aliyejurehuwa na bomu akatwa kiganja

Aliyejurehuwa na bomu akatwa kiganja

Mkazi wa Mbagala Zakhiem, Mwanaharusi Hamis amepoteza kiganja chake cha mkono wa kulia baada ya kulipuliwa na kitu kinachodaiwa kuwa ni bomu lililorushwa na polisi wakati wakitawanya wananchi.
Mwanaharusi alilipuliwa na bomu hilo Agosti Mosi 2014, saa 3:00 usiku alipokuwa anatoka ndani kwenda msalani.
Akizungumza na gazeti hili jana katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, Wodi ya Mwaisela namba mbili alikolazwa, alisema tukio hilo limebadilisha kabisa mustakabali wa maisha yake.
Mwanaharusi, ambaye ni mama wa watoto wawili alisema alikumbwa na madhila hayo wakati polisi walipokwenda mtaani kwao kumkamata mtuhumiwa wa wizi wa pikipiki. Alisema walipofika, vijana waliokuwa maeneo hayo waliwarushia polisi mawe, ndipo polisi walipofyatua mabomu ya machozi na risasi kuwatanya wananchi hao.
“Ilikuwa saa 3:00 hivi mimi na watoto wangu tukiwa ndani hatujui nini kinachoendelea nje, ghafla tulianza kusikia milio ya risasi na mvumo wa kitu kuelekea upande wa ilipo nyumba yetu. Wakati huo nilikuwa natoka ndani kwenda msalani, nikaona kitu kimenipiga na kunichana sehemu za mkono na miguuni, baadaye nikagundua kilichonipiga kilikuwa bomu,” alisimulia Mwanaharusi.
Alisema baada ya tukio hilo polisi walimpelekea kituoni kwa ajili ya kupata fomu namba ya tatu ya matibabu (PF3) na baadaye Hospitali ya Temeke, alikopewa rufaa ya kwenda Muhimbili kwa kuwa alikuwa akitoka damu nyingi.
“Nimechanganyikiwa. Mimi ndio mtafutaji wa familia, mwanangu wa kwanza amemaliza kidato cha nne na wa pili ana miaka tisa,” alisema.
Kamanda wa polisi wa Mkoa wa Temeke, Kienya Kienya alikiri kutokea kwa tukio hilo na kusema ufafanuzi utatolewa leo na kamanda wa Kanda ya Dar es Salaam, Kamishna Suleiman Kova.
Share this article :
 
Copyright © March 2012. MARIDADI AGENCY
-Haki zote zimehifadhiwa
- All Rights Reserved
Template Modified by Hassan Moh Toziri
Published by Maridadi Agency